|
MKENYA AMUUZA ALBINO KWA MIL.400....SCARY.... |
|
Written by Mange
|
|
Tuesday, 17 August 2010 19:31 |
|

Raia wa Kenya Nathan Mtei anayetuhumiwa kumleta nchini mlemavu wa ngozi(albino) Robinson Mkwana Mnyoti (hayupo pichani) ili kumuuza jijini Mwanza. (Picha na Clara Matimo).
BAADA ya wimbi la mauaji ya albino kwa ajili ya kuuza viungo vyao kudhibitiwa na Jeshi la Polisi nchini, mbinu za wauaji zimebadilika na sasa wameanza kuwauza wakiwa hai. Hali hiyo imedhihirika baada ya polisi mkoani hapa kufanikiwa kumnasa raia wa Kenya akituhumiwa kumsafirisha albino kutoka nchini mwake hadi jijini hapa kwa lengo la kumuuza. Mkenya Nathan Mtei (28) hivi sasa anashikiliwa na Jeshi hilo mjini hapa kwa tuhuma za kumsafirisha binadamu mwenzake, albino Robson Mkwana Mnyoti (20) kwa lengo la kumuuza. Kamanda wa Polisi wa Mkoa Simon Sirro, jana alithibitisha tukio hilo na kusema, “ni kweli tunamshikilia Mtei tangu Agosti 15 mwaka huu alipokamatwa saa 10 jioni akihusika na tuhuma za kufanya biashara ya viungo vya albino.” Sirro alifafanua kuwa walipata taarifa kutoka kwa raia wema na askari wakajifanya wanunuzi wa viungo vya albino. "Tulipata namba yake na tukampigia Mtei akatuahidi kuwa atafika nchini Agosti 12 mwaka huu akiwa na ‘mzigo’, ni kweli alifikia hoteli moja (jina tunalo) iliyopo Nyakato na tulipokwenda akaomba Sh milioni 400 ili aweze kutupa viungo hivyo,” alisema Kamanda Sirro. Aliongeza kuwa baada ya kutoa hizo Sh milioni 400 walishangaa kuona wanakabidhiwa binadamu hai na kuambiwa waende wakashughulike naye wenyewe. Alisema baada ya kumhoji mtuhumiwa, alikiri kuwa kweli hufanya hiyo biashara ya viungo vya albino ingawa hakuwa tayari kusema amekwishafanya mara ngapi. Kamanda Sirro alifafanua kuwa Mtei alimchukua Mnyoti kwa makubaliano kuwa anamleta Tanzania kumtafutia kazi ya udereva, lakini haikuwa hivyo. Kamanda alisema mtuhumiwa atafikishwa mahakamani leo kujibu mashitaka yanayomkabili. Tanzania iligubikwa na mauaji ya albino na viungo vyao kuuzwa kwa imani za kishirikina, kwamba vikitumiwa vinaweza kusababisha utajiri. Hivyo wavuvi na wachimbaji madini walikuwa wakiaminika kujiingiza katika imani hizo na kusababisha mauaji hayo kukithiri, huku baadhi ya albino wakinyofolewa viungo wakiwa hai na kuachwa na ulemavu wa kudumu. Hata hivyo, Serikali iliamua kulivalia njuga suala hilo na baadhi ya watu kufikishwa mahakamani na baadhi yao kuhukumiwa vifo.(Picha na stury from Habari Leo)
|